Changi N'Kuchangizana Tungo Za Kiswahili |
|
Author:
| (Mhariri), Mohammed |
ISBN: | 978-1-5375-3014-7 |
Publication Date: | Sep 2016 |
Publisher: | CreateSpace Independent Publishing Platform
|
Book Format: | Paperback |
List Price: | USD $7.00 |
Book Description:
|
Ushairi ni sauti ya ndani. Ndani kabisa huko moyoni na huko kwenye chumba cha ndani cha ubongo, ambako mshairi hujisemesha na kuusemesha ulimwengu wake na wa wenzake. Ushairi ni hisia na pia ni fikira ya ndani. Kwa kuwa kwake sauti ya ndani, kunaufanya uwe kielelezo cha fikra huru za mwanaadamu, kwani huwa anajisemesha akiwa peke yake, pasina na nguvu za nje anazozikhofia kumsakamiza matambara mdomoni. Mshairi ni ndege aamkaye kiotani mwake asubuhi na mapema, akayatumbuiza mandhari kwa...
More DescriptionUshairi ni sauti ya ndani. Ndani kabisa huko moyoni na huko kwenye chumba cha ndani cha ubongo, ambako mshairi hujisemesha na kuusemesha ulimwengu wake na wa wenzake. Ushairi ni hisia na pia ni fikira ya ndani. Kwa kuwa kwake sauti ya ndani, kunaufanya uwe kielelezo cha fikra huru za mwanaadamu, kwani huwa anajisemesha akiwa peke yake, pasina na nguvu za nje anazozikhofia kumsakamiza matambara mdomoni. Mshairi ni ndege aamkaye kiotani mwake asubuhi na mapema, akayatumbuiza mandhari kwa njia za kuyasawiri, kuyasema, kuyasemea, na kuyatarajia, bali hata kuyasuta na kuyakosoa. Mshairi ni wimbi la bahari livumalo katikati ya mkondo na mto utiririkao milimani, ukipenya mule ambamo wenda kwa miguu wa kawaida, hawawezi kumupita. Mshairi ni maji ya mvua inyeshayo kutononesha ardhi, na pia mshairi ni jua liwakalo kukausha vilivyo juu ya ardhi hiyo. Kwa bahati mbaya, hata hivyo, si kila ushairi unaoimbwa ndani ya nafsi ya mshairi hubahatika kuja kuimbwa hadharani ama kuwekwa maandikoni. Daima tungo zilizotungwa ni nyingi zaidi kuliko zile zilizowahi na zitakazowahi kutufikia sisi, hadhira, katika vipindi vyote vya historia ya mwanaadamu. Hutokea sadfa tu kwamba baadhi ya tungo hizo hupata nafasi ya kuhifadhiwa na kusambazwa, zikaenda mbali, nje ya jengo la nafsi la mshairi mwenyewe, na kufika pa kufika. Sadfa hiyo huufanya ushairi kutoka kwenye kilango chake cha ndani na kuwa nyimbo ya kughaniwa kweupeni - jahara shahara - pa kila mtu kuusikia na kuuhisi. Lakini ushairi si kila sauti ya ndani ajisemeshayo mshairi tu, maana mshairi naye ni mwanaadamu, ambaye mawasiliano yake mengine huwa si ya kishairi. Anapouvaa ushairi wake, ndipo hapo anapotoa na kutumia sauti yenye upekee; kwanza, kutokana na mapigo yake, kwa ule muziki na mahadhi yake; na, pili, ni kwa uzito wa ujumbe wake, upeo wa fikra zake na ule ujuzi wa mafunzo yake. Ushairi ni sauti ya furaha kama ilivyo ya huzuni, ni sauti ya hasira kama ilivyo ya nasaha, ya kupongeza kama ilivyo ya kulaumu, ya kuagiza kama ilivyo ya kuitikia maagizo. Alimradi, katika undani wa dhati yake, ushairi husimama kama kauli inayojitegemea na kujipambanua.